.

.

Ugomvi wa wazazi, baba amvunja mguu binti yake

mtoto avunjwa mguu na baba (3)Mtoto  Zainabu Shaban akiwa na magongo.
Na Gladness Mallya, UWAZI
DAR ES SALAAM: Ni shida! Mtoto  Zainabu Shaban, 16, (pichani) mkazi wa Kimara-King’ong’o, Dar amejikuta katika wakati mgumu baada ya kudaiwa kuvunjwa mguu na baba yake mzazi wakati wakiwa kwenye ugomvi na mama yake kisa kikitajwa mchepuko.
Akizungumza na gazeti hili, Zainabu alidai siku ya tukio baba na mama yake walikuwa  wana ugomvi  akaamua kukimbilia kwa jirani yao ambapo alilala huko na kurudi nyumbani kesho yake na kujiandaa kwenda shule kwani anasoma kidato cha pili.
mtoto avunjwa mguu na baba (1)Baba yake mzazi wa Zainabu, Shaban.
Jioni alirudi nyumbani na kumkuta baba yake akiwa ameandaa fimbo kwa ajili ya kumchapa kisa, jana yake alikwenda kulala kwa jirani hivyo alipoingia tu ndani alimpokea na kumtaka alale chini ili amuadhibu, akatii amri hiyo ikawa anachapwa ndipo mama yake alipoingilia kati baada ya kuona anaumizwa kwa sababu fimbo ilikuwa kubwa.
“Mama aliingilia ambapo baba alimgeukia na kumpa kipigo ikabidi ninyanyuke pale nilipokuwa nimelala na kuwaamua, baba akanigeukia tena kutaka kunipiga ikabidi nikimbie lakini nilijikwaa kwenye mlango naye akaja akanikanyaga mguu, ukavunjika, kiukweli naumia sana na sitaki hata kumuona baba maana amenipa kilema,” alidai Zainabu.
mtoto avunjwa mguu na baba (2)
Zainabu akiwa na mama yake.
Naye Mama Zainabu alieleza kuwa mumewe ndiye aliyemvunja mtoto wao mguu na ilikuwa ni kwenye ugomvi kati yake na mumewe baada ya kumwambia aachane na mchepuko ambao unamzuia kutoa matumizi muhimu kwa watoto wanne. “Ugomvi na mume wangu umekuwa ni wa kila siku sababu kubwa ni kwamba ana mchepuko na mwanamke mwenyewe namfahamu na hivi karibuni niliwafuma nikamshushia kipigo sana huyo mwanamke, hatoi matumizi nyumbani na mara mojamoja ndiyo anaacha shilingi elfu mbili ambazo hazitoshi chochote, amemvunja mwanangu mguu lakini hataki hata kumhudumia, nauza matembele ndiyo napata nauli ya kumpeleka Hospitali ya Muhimbili.
“Mume wangu siku ya ugomvi nilimshauri tu aachane na huyo mwanamke kwani kama kipato chake ni kidogo anapata wapi fedha za kumpa, ndipo ugomvi ulipoanzia na kusababisha matatizo yote haya.
“Alikamatwa na polisi akakaa huko siku kadhaa nikaenda kumwekea dhamana ili tuje kusaidiana matibabu lakini hakuna anachonisaidia,” alidai mama huyo.
Baba wa mtoto huyo, Shaban alipotafutwa alikiri kutokea kwa ugomvi huo na kumpiga mwanaye lakini suala la kumvunja mguu alikanusha.
“Mke wangu anasema uongo, huyo mtoto alianguka mwenyewe wakati anakimbia nisimchape, kipato changu ni kidogo na matumizi ya nyumbani natoa lakini mke wangu haridhiki na hicho kidogo, naumia sana wanavyonisingizia nimemvunja mguu mtoto wangu na kuwa na mchepuko,” alisema Shaban.
Mwenyekiti wa mtaa wa eneo hilo, Demetrius Mapesi alithibitisha kutokea kwa tukio hilo. “Mtuhumiwa yaani baba wa Zainabu alifikishwa katika Kituo cha Polisi Kimara na kufunguliwa kesi namba KMR/RB/1822/2016 KUSHAMBULIA, lakini baadaye alitolewa kwa dhamana,” alisema.
Share on Google Plus

About UPStream Telecom

0 comments:

Post a Comment