MABOMU ya machozi jana yalipigwa nje ya Uwanja wa Taifa jijini Dar es
Salaam kuwatawanya mashabiki wa soka waliokuwa wakilazimisha kuingia
uwanjani kushuhudia Yanga ikicheza na TP Mazembe ya Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Mashabiki wa soka walianza kuingia uwanjani mapema asubuhi na
ilipofika saa tano asubuhi tayari uwanja ulikuwa umejaa pomoni na askari
walianza kuzuia watu wasiendelee kuingia uwanjani.
Sehemu ya viti vya wageni mashuhuri (VIP) pekee ndio ilikuwa na
nafasi na iliachwa mahsusi kwa ajili ya wageni maalum wa timu hizo
pamoja na wale wa serikali.
Lakini tukio la mashabiki kuzuiwa baadhi yao hawakukubaliana nalo,
hivyo kulazimisha kuingia ndani kwa nguvu. Kutokana na hali hiyo ilibidi
polisi kutumia mabomu ya machozi majira ya saa sita mchana muda mfupi
baada ya kutangaziwa kwamba uwanja ulikuwa umejaa.
Licha ya tukio hilo la polisi, lakini baadhi ya mashabiki hao wengi
wao wakiwa vijana waliendelea kung’ang’ania kutaka waingie uwanjani.
Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Alfred Lucas alituma
ujumbe katika vyombo vya habari kuomba watangaze wananchi wasiende
uwanjani maana ulikuwa umejaa.
“Naomba wananchi ambao wapo njiani kuja uwanjani wasije uwanja umejaa
tayari na mageti yamefungwa. Pia wale waliopo nyumbani wabaki
hukohuko,” alisema Lucas majira ya saa sita mchana jana.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro aliingia
uwanjani hapo majira ya saa 7;30 mchana kuangalia hali ya usalama na
baadaye kupanda jukwaa la VIP.
Kivutio kingine kikubwa jana ilikuwa mashabiki wa TP Mazembe ambao
wakati wanaingia uwanjani walishangiliwa kwa kiasi kikubwa na mashabiki
wa Simba. Mashabiki wa Yanga walijitahidi kwa kiasi kikubwa kuihamasisha
timu yao jana kwa kuishangilia kwa nguvu, lakini matokeo hayakuwa
mazuri kwa upande wao.

0 comments:
Post a Comment